Pages

Saturday, 3 August 2013

Huu ndio Upande wa Pili wa Suarez wa Arsenal

 


Hii ni kwa shabiki wa Arsenal. Hebu kaa kimya, kwa sekunde chache tu, kisha jiulize. Ingekuwa vipi Luis Suarez angekuwa Arsenal kwa sasa? Ungetaka abaki, au aende zake huko anakohitajika? Usijibu.
Mengi yanasemwa katika kipindi hiki, hasa baada ya Arsenal kupeleka ofa ya pauni 40,000,001 Liverpool, wakimtaka straika huyo, Suarez. Hakuna shaka, shabiki yeyote wa Arsenal ni mtu mwenye furaha kubwa kwa sasa kwasababu klabu yao inafukuzia usajili wa moja ya wanasoka wenye vipaji kwenye soka la kisasa.
Na zaidi ya hilo, Suarez amekuwa fundi mzuri wa kufunga mabao. Anafanya hivyo kila anapocheza. Lakini, linapokuja suala la kutaka kumsajili, Arsenal pamoja na furaha yao yote, inapaswa kujiuliza maswali ya msingi. Anafaa au usajili wake unataka kufanywa kwa kujikosha tu kwa watu kuwa nao wanasajili wachezaji wenye majina?
Ingekuwa vipi, Suarez kwa sasa angekuwa mchezaji wa Arsenal na analazimika kuhama? Tena angekuwa analazimisha kuhamia kwa timu kama Manchester City? Msimu uliopita, Robin van Persie alihamia Manchester. Mashabiki wengi sana wa Arsenal walikasirishwa na hilo, kwa sababu moja tu. Walimvumilia wakati wa majeruhi, walimsapoti kwa kila kitu na kisha akawaacha na kwenda kwa wapinzani, Manchester United. Haikuwa vizuri kwa mashabiki wa Arsenal kwa uamua wa kuhamia Manchester United.

Na mbaya zaidi alifanya hivyo baada ya msimu mmoja kucheza kwa kiwango kikubwa, bila ya kusumbuliwa na majeruhi yoyote. Hili halina tofauti sana na hadithi ya Suarez. Misimu miwili iliyopita, Suarez amekuwa mtuhumiwa wa matukio ya utovu wa nidhamu ndani na nje ya uwanja, lakini bado klabu yake ilimsapoti kwa kila hali. Baada ya kuandamwa na vyombo vya habari, straika huyo aliibuka na wazo la kutaka kuhamia ng’ambo ya nchi.
Lakini, baadaye akadai kwamba anataka kujiunga na timu itakayompa nafasi ya kucheza Ligi ya Mabingwa Ulaya bila kujali kama itakuwa ndani ya England au la. Kesi ya Suarez ipo tofauti na ya Van Persie, mshambuliaji huyo wa Uruguay ni mbinafsi, anajifikiria yeye zaidi. Kwa tabia yake hiyo, Arsenal wanapaswa kujiuliza kabla hawajatoa pesa yao nyingi kumsajili.
Arsene Wenger hapaswi kusahau kwamba ni Real Madrid, ambayo ni chaguo la kwanza la Suarez. Si Arsenal. Pia fikiria hili, Suarez ametua Arsenal, akaisaidia kutwaa taji la Ligi Kuu na kisha akafunga mabao 30. Unadhani kuna uhakika atabaki Arsenal mchezaji huyu? Mchezaji ambaye mapenzi yake ya kwanza yapo kwingine? Anadhani atazikataa Real Madrid na Barcelona zitakapokuja na ofa zao kutaka kumsajili?
Suarez ni mchezaji mahiri kweli, hilo halina pingamizi. Lakini, kwanini Wenger hakumsajili mchezaji huyo wakati alipokuwa Ajax. Kwa shabiki wa Liverpool uhamisho wake utamfanya kuwa na hasira, kwa sababu anahama baada ya kupata sapoti kubwa ya matatizo yake yenye utata. Kwa upande wa Arsenal, ukiweka ushabiki pembeni, kumsajili Suarez ni kujiweka katika hali ya hatari. Ikumbukwe, atahamia hapo akiwa na adhabu ya kukosa mechi sita. Je, kuna uhakika kwamba amepona ugonjwa wake na hatamng’ata mchezaji mwingine atakapokuwa ndani ya jezi za Arsenal?
Je, hatakumbana na adhabu ndefu wakati atakapotua Emirates? Je, hataamsha tena sakata la kutaka kuhama baada ya misimu miwili hasa ukizingatia mapenzi yake si kuichezea Arsenal? Kwa Suarez, Arsenal inajitengenezea bomu, itamsajili kwa pesa nyingi na kisha baada ya miaka miwili ataomba kwenda Barcelona au Real Madrid. Sawa, humtarajii Suarez azekee Emirates, lakini itakuwa hasara kama ataomba kuondoka baada ya misimu miwili.
Huu ndio wasiwasi  wa kuwa na mchezaji kama Suarez, ana uwezo lakini hakupi uhakika wa kuwa na mipango ya kujenga timu kupitia yeye. Real Madrid na Barcelona bado zitaendelea na chokochoko zao za kumsajili kama ataendeleza makali yake atakapotua Emirates.   
     
Kwa kiwango cha Suarez, kama hajapata tatizo la majeraha, suala la kung’ara hilo halina mjadala. Unatarajia kuliona kutoka kwake. Hakuna ubishi Arsenal itakuwa imepiga  bao watakapoinasa huduma yake, lakini tatizo lake ni moja tu. Haaminiki, hakawii kuchafua hali ya hewa. Hili ndilo lililopo upande wa pili wa sarafu katika usajili wa Suarez Arsenal.

source: mwanaspoti.co.tz



No comments:

Post a Comment